Jumapili moja nilikuwa kanisani nikimsikiliza Mhubiri. Mhubiri huyo alitoa mfukoni noti za shilingi elfu kumi kumi zilizokuwa na jumla ya shilingi laki moja, akauliza: “Ni nani miongoni mwenu anataka nimpe hii laki moja?”
Watu wengi waliokuwa mle Kanisani walinyoosha mikono, kila mmoja alikuwa akipiga kelele ya “Mimi! Mimi!”. Nikaanza kushangaa ni nani atakuwa na bahati ya kupewa ile pesa kati ya mamia ya watu waliohudhuria ile ibada. Pia nikajiuliza kwanini (ambapo bila shaka na baadhi ya wengine nao walijiuliza) atoe kitita cha shilingi laki moja kirahisi rahisi hivyo!
Wakati watu wakiendelea kupiga kelele kusema “nipe mimi, nipe mimi” huku wamenyoosha vidole vyao, kutokea nyuma akaibuka msichana mdogo mwenye umri kama miaka 14 hivi, akaenda mbele kule aliko yule Mhubiri akafika mbele na kuchukua ile laki moja kutoka mkononi mwa yule Mhubiri.
“Safi sana, msichana! Umefanya vema,” alisema yule Mhubiri.
“Wengi wetu tunapenda kukaa tu na kusubiri mambo mazuri yaje yenyewe. Hii haitaweza kuwasaidia hata kidogo, unatakiwa kuinuka na kutafuta mafanikio. Mafanikio hayawezi kuja kama umekaa tu.”
Na maisha yetu ndivyo yalivyo, tunaziona fursa nyingi sana zikiwa zimetuzunguka, kila mtu anahitaji mambo mazuri. Ila tatizo hatutaki kusimama na kuzifuata hizo fursa. Simama sasa na ufanye kitu, usisubiri mafanikio huku umekaa, kamwe hayatakuja.
Usijali watu watasema nini. Chukua hatua…