Hongera sana Wabunge wa Chadema

UPINZANI WAHENYESHA MAWAZIRI, AG BUNGENI
http://mtanzania.co.tz/wp-content/uploads/2018/09/bunge-LIVE-300x158.jpg
*Waziri kivuli wa elimu atumia saa moja na nusu kufumua Muswada wa Bodi ya Walimu
*Serikali yakubali marekebisho sita kati ya 10, aliyoyawasilisha
Na ESTHER MBUSSI,DODOMA

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imeihenyesha Serikali kwa saa moja na nusu wakati Bunge lilipokaa kama kamati kupitisha Muswada wa sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania wa Mwaka 2018.
Waziri kivuli wa Wizara ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Suzan Lyimo (Chadema), alitumia zaidi ya saa moja na nusu kubishana na Serikali akiwa na marekebisho ya vifungu 10 vya muswada huo.

Majibizano hayo ya kisheria yalianza saa 5:29 asubuhi na kumalizika saa 6:50 mchana, ambapo hoja sita za Lyimo zilikubaliwa.
Katika majibizano hayo, Lyimo alikuwa akibishana na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako na Naibu wake, Gabriel Ole Nasha, Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk. Adelardus Kilangi na Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Azzan maarufu Zungu.
Kati ya marekebisho 10 yaliyowasilishwa na Lyimo mawili yakikataliwa na pendekezo moja aliliondoa mwenyewe kama alivyotakiwa na mwenye ambayo hata hivyo alidai yalikuwa yana mkanganyiko na halina mashiko.

HALI ILIVYOKUWA
Mara ya kipindi cha maswali na majibu kwish, Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini, aliomba mwongozo wa kiti ili wabunge wapewe nafasi ya kuchangia tena kwa sababu muswada huo ulipangwa kwenye ratiba kujadiliwa kwa siku mbili ambapo hata hivyo Zungu aliikata hoja hiyo na kuruhusu mawaziri kujibu hoja hizo.
Maaba ya majibu ya mawaziri na bunge kuketi kama kamati, Lyimo alisimama na kukuomba marekebisho ya muswada huo kwa kutaka Mwenyekiti wa bodi hiyo awe mwalimu kitaaluma na pia ujuzi wa miaka 10 ambapo katika muswada ilionyesha mwenyekiti anaweza kuwa mtu yeyote aliyesomea ualimu.
Akinukuu kifungu hicho, alisema kinasema; “A chairman who shall be appointed by the president from among registered among the Senior professional” na kuongeza kuwa kifungu hicho hakijaeleza miaka ya mtu kuitwa Senior, ndiyo maana anapendekeza kuwa mwenyekiti atakayeongoza awe na uzoefu wa kufundisha miaka 10.
“Huwezi mtu ukaingia leo kazini alafu ukawa Senior, unapata uzoefu wakati umeshakaa katika kiti, na ndiyo maana kuna Junior na Senior, haiwezekani mtu afanye kazi miaka mitatu ukasema ni Senior kuliko aliyefanya kazi miaka 15, suala hili ni muhimu naomba tulijadili,” alisema.
Akijibu hoja hiyo Naibu Waziri wa Elimu, Ole Nasha alisema Serikali imeona ibakie kama ilivyokuwa kwa sababu tayari kwenye utumishi wa umma kuna madaraja ya ualimu kwa hiyo haiwezekani kuweka kipengele kipya ya mwalimu ambaye ana uzoefu wa miaka fulani maana yake wanametengeneza daraja ambalo lipo kwa hiyo wanapendekeza ibakie kama ilivyo.

Baada ya Ole Nasha kujibu hayo, Zungu alimuita tena Lyimo ambaye alikataa hoja hiyo akisema; “Bodi hii pamoja na mambo mengine ni kitu kipya kabisa ambacho kinawaleta walimu hata wa sekta binafsi na kama madaraja yapo nafasi hiyo, haiwezekani ukasema tu ni senior walau kuwe na ujuzi na hii inatuhakikishia kwamba hamuwezi kumleta mtu wa sekta binafsi kwa sababu hajatoka sekta binafsi hii si sawa.”
Hoja hiyo ilimuibua Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye alisema inapendekezwa msimamo wa Serikali kubaki huo huo kwa sababu kipindi cha kufundisha miaka mitano au 15, huo ni uzoefu na huo haukidhi kuwa taaluma, taaluma ya mwalimu inatokana na mafunzo ya ualimu.
“Kwa hiyo kipindi cha mwaka mmoja, miwili au mitatu hiyo inaitwa uzoefu, na hatupendi kuchanganya uzoefu na taaluma,” alisema Dk. Kilangi.
Hata hivyo, uliibuka utata wa neno uzoefu na taaluma ambapo Lyimo akichangia tena alisema anapata tabu kati ya maneno hayo na kuongeza kuwa haiwezekani ukawa senior kama hujafanya kazi.

Alisema huwezi ukaingia leo kazini kisha ukawa senior ambayo unaweza kuipata baada ya kufanya kazi kwa muda mrefu na kinachomwongezea sifa ni hicho.
Hoja haya hiyo iliungwa mkono na Mbunge wa Viti Maalumu, Ruth Mollel (Chadema), ambaye alisema mtu anayekuwa senior ni mtu aliyefanya kazi kwa muda fulani kutokana na muundo wa utumishi, kwa hiyo taaluma ni kwa sababu ya hiyo kazi anayofanya ambapo pia aliomba marekebisho hayo yafanyike.
Akichangia hoja hiyo Mbunge wa Ileje, Janeth Mbene (CCM), alisema seniority inaweza kutokana na vigezo vya taaluma ambapo mtu anaweza kuwa na miaka mingi kwenye kazi lakini ujuzi wake ukawa chini.
Alisema mtu kama huyo huwezi kumuita senior ambapo aliomba ibakie kama ilivyo kwenye muswada. hoja iliyoungwa mkono na Mbunge wa Hanang, Mary Nagu (CCM).

Naye Mbunge wa Jimbo la Mchinga (CUF), Hamidu Bobali, aliunga mkono hoja ya Lyimo na kuongeza kuwa mtu anaweza kuwa na vigezo lakini asiwe na ujuzi wa kazi.
“Naunga mkono hoja ya Lyimo, unaweza kuwa na vigezo lakini ukakosa ‘experience’ (ujuzi), na ndiyo maana tumeweka madaraja ya walimu, ambayo yanapanda kulingana na experience na miaka ya kufanya kazi,” alisema.
Akijibu hoja hiyo Ole Nasha alisema si kwamba Serikali inaikataa hoja hiyo isipokuwa huu si wakati sahihi kwa sababu ameleta neno jipya kwenye tafsiri ya muswada na kwamba wanataka kujadili seniority ya walimu mjadala huo unatakiwa utoke baada ya hapo na serikali iko tayari kuwashirikisha walimu au kuirekebisha baadaye sheria hiyo. Hata hivyo kifungu hicho kilikataliwa.

Aidha, katika kifungu cha tano Lyimo alisimama tena kuomba kifanyiwe marekebisho katika neno ‘Chairman’ na kuwa ‘Chaiperson’ ili kuleta usawa wa kijinsia hata hivyo, Dk. Kilangi alisema kwa mujibu wa sheria neno hilo bado linabaki hivyo ambapo kwa utaratibu linatumika hivyo.
Baadhi ya mambo yaliyochukuliwa na serikali ni lile la nyongeza ya sifa za usajili ambayo ni kusajili walimu taaluma ya ualimu ambapo alisema haiwezekani leo unasajili mtu kwa taaluma hii kesho unabadili kwani watu wanahitimu kila siku kwa hiyo lazima kuwe na wastani wa usajili.
Suala la kumsajili mwalimu kwa kumtangaza kwenye gazeti la serikali ambapo kwenye kwenye muswada ilitaka mwalimu anaposajiliwa atangazwe kwenye gazeti la Serikali ambapo akifukuzwa anatakiwa kutangazwa kwenye magazeti mengine ambapo katika mapendekezo yake Lyimo alisema kufanya hivyo ni kumdhalilisha mwalimu kwamba kwanini wakati wanamsajili anafichwa lakini anapofukuzwa atangazwe.

Hongera kwa suzani.japo hadi sasa bado sijapata hoja hasa ya huo usajiri wa walimu